KISWAHILI: Kuhakiki riwaya ya Rosa Mistika


Hakiki riwaya ya Rosa Mistika (Euphase Kezilahabi) kwa kutumia nadharia ya U-Marx.
 
Katika utangulizi tutaanza kuelezea maana ya nadharia kutokana na wataalam mbalimbali walivyoielezea, tutaangalia maana ya U-marx kutokana na wataalam mbalimbali. Na tutajikita katika kuelezea misingi ya uhakiki wa ki-marx,  kwa kutumia misingi hiyo tutahakiki  riwaya ya Rosa Misitika na mwisho tutamalizia na hitimisho.

Nadharia ni dhana iliyofafanuliwa na wataalam mbailimbali kama ifuatavyo:-

Wafula na Njogu(2007) wanaeleza kuwa nadharia ni “jumla ya maelekezo yanayomsaidia msomaji au mhakiki kuifahamu kazi ya fasihi kwa kufuata utaratibu maalumu.” TUKI (2004) wanasema  nadharia ni “mawazo, maelezo au muongozo ili kusaidia kueleza,kutatua na kutekeleza jambo fulani.” Hii ina maana kuwa msomaji kupitia nadharia anapata uwezo wa kufahamu mambo mengi kwa undani ambayo anaweza kuyatumia katika kazi yake ya kifasihi.

Hivyo basi nadharia ni taalumu inayojishughulisha na uchambuzi na uchanganuzi juu ya asili au mwazo wa kitu au jambo fulani.

Dhana ya U-marx imeelezwa na wataalamu mbalimbali kama ifuatavyo;Wamitila(2006) anasema U-marx ni falsafa ya kiyakinifu hasa kwakuwa pana msisitizo mkubwa kwenye msingi wa hali za kiyakinifu za maisha kama mazingila ya kuishi kuliko mawazo katika maisha ya binadamu. Ikimaanisha kwamba mawazo yake hayategemezi kwenye dhana dhahania kama urembo,ukweli au ndoto bali anayategemeza kwenye uhalisia unaonekana. Nadharia ya U-marx ilianzishwa na Karl Marx mwaka 1818-1863 na Fredrick Engles mwaka 1820-1895.

Katika kutekeleza  nadharia ya U-marx kuna misingi  ya kufuata ili kuhakiki kazi za kifasihi kwa ufasaha. Moja, misingi hiyo ni historia ya maisha ya binadamu inayoweza kuelekeza katika misingi yakinifu ya kiuchumi; ambayo itachunguza njia ya uzalishaji mali pamoja na miundo ya kiuchumi inayo athiri uzalishaji mali na usambazaji wa mali hizo. Pili, kuamini kuwa historia ya kibinadamu inadhihirisha au kuakisi harakati zinazo endelea katika matabaka ya kiuchumi-jamii; matabaka hayo yapo katika ngazi ya familia, dini na elimu na tatu, ubepari kama njia ya uzalishaji mali na mara nyingi huharibiwa na tabaka la chini.

Kulingana na misingi ya  ki-marx , tunaweza kuhakiki Riwaya ya Rosa Misitika iliyoandikwa na Euphrase Kezilahabi  kama ifuatavyo:-


 Suala la dhuluma na unyanyasaji; unyanyasaji ni kitendo cha mtu mwenye nguvu au shirika fulani kuwakandamiza watu wasio na nguvu katika familia au  jamii fulani inayowazunguka na dhuluma ni kitendo cha mtu au watu kunyimwa haki zao za msingi. Kupitia msingi wa nadharia ya ki-marx inaonesha suala la ubepari kwamba ni jumuisho katika suala la dhuluma na unyanyasaji. Mwandishi anawatumia wahusika Flora, Stella, Honorata, Sperantia na Emmanuel walivyodhulumiwa  kwa kunyang’anywa vitu vyao  vyote baada ya wazazi wao kufariki. Katika uk.96,  msanii anasema:-

“Hawa  jamaa walirithi. Walirithi hawa jamaa. Walirithi, walirithi. Jamaa waligawana vitu. Walirithi kila kitu kilichokuwa ndani ya nyumba. Walirithi michungwa na miembe. Walirithi migomba yote. Walirithi paka na mbwa. Walirithi majani yaliyokuwa juu ya paa, na miti yote, iliyofanya nyumba isimame. Walirithi mashamba yote. Walirithi kuku, kweli walirithi. Lakini hapakuwa  na mtu hata mmoja aliyeweza kusema atamchukua mtoto fulani amtunze.”

Vilevile msanii anaonesha suala la unyanyasaji   kwa kumtumia mhusika Regina anavyonyanyaswa na mumewe. Mfano katika riwaya ya Rosa Mistika suala la unyanyasaji limejitokeza katika sehemu ya kwanza uk. 3 mwandishi anaposema:

‘‘Lakini Regina tangu aolewe hakuwa na raha ;alikuwa akisumbuliwa na kuteswa na mumewe kwa kosa lisilo lake.”

 Wanawake  wengi  katika jamii zetu  wamekuwa wakinyanyaswa na waume zao kwa kupigwa na kupewa majukumu yote ya familia bila ya kusaidiwa na waume zao.

Nadharia ya u-marx inazungumzia suala la unyanyasaji na dhuluma kuwa ni tatizo kubwa katika jamii hasa katika kufanya maendeleo ya kijamii ili  jamii iweze kujikomboa  kiutamaduni ,kisiasa na kiuchumi.  

Vilevile  suala la uongozi mbaya, uongozi mbaya ni kitendo cha viongozi kushindwa kukidhi mahitaji ya watu wake. Pia suala hili la uongozi mbaya ni moja kati ya suala zima la ubepari ambalo huleta mikururo katika jamii, hivyo mwandishi anaonesha uongozi mbaya kwa kumtumia mhusika Deogratias pale anapo kuwa anatumia cheo chake vibaya kwakuwa kandamiza watu. Uk. 41 mwandishi anasema:-

“Zaidi ya hayo,Deogratias alikuwa mmoja kati ya wale watu watumiao vyeo vyao na pesa kwa kutaka chochote wapendacho.”

“...Nasikia alikwisha wapa mimba watoto wawili wa shule? Ndiyo, lakini aliwapa shilingi wasimseme. Walitaja vijana wengine waliokuwa wakisoma nao.”

Pia suala la uongozi mbaya lipo hata katika jamii zetu kwani kuna baadhi ya viongozi ambao hutumia nafasi zao kufanya vitu visivyostahili katika jamii mfano rushwa ya ngono, matumizi mabaya ya fedha za serikali.

Katika nadharia ya U-marx inasema kwamba ili jamii iondokane na uongozi mbaya ni lazima jamii  ipambane kuondoa  uongozi mbaya.

Pamoja na hayo  suala la migogoro mwandishi amelionesha; migogoro ni mvutano au ukinzani baina ya mtu na mtu au pande mbili. Migogoro imegawanyika katika makundi mbalimbali mfano migogoro ya kinafsi, mtu na mtu, mtu na serikali au jamii yake. Katika riwaya hii mwandishi anaonesha jinsi jamii ya watu wa Ukerewe wanavyokumbwa na mikururo katika jamii hiyo. Mwandishi anamtumia mhusika Rosa anavyokua na mgogoro na baba yake kutokana na malezi  aliyokuwa anapewa na baba yake.  Katika uk. 58  mwandishi anasema:-

‘’Zakaria alipata maneno yote: maneno aliyopaswa kuambiwa siku ile……Rosa tangu leo wewe si mototo wangu. Tangu leo wewe si baba yangu. Rosa alidakia bila kukawia. Aliingia mara moja ndani ya motakaa na kwenda zake Beach. Siku hiyo Rosa hakurudi nyumbani.”

Suluhisho la mgogoro huu ni Rosa kuondoka na kutokurudi nyumbani.

Mgogoro mwingine ni kati ya Regina na Zakaria kutokana na  suala  la ulevi wa Zakaia ambae ni mume wa Regina. Uk. 4. Mwandishi anasema:-

‘’Mwanzoni haya yalikuwa yakizunguka kichwani mwake aliposikia sauti kwa mbali: Hoi! Hoi! Hoi! Alifahamu. Alifahamu huyo mtu alikuwa nani na alikuwa katika hali gani: sauti hiyo alikwishaizoea.’’

Mgogoro huu haukupatiwa suluhisho kwani Zakaria aliendelea na tabia yake ya ulevi mpaka mauti yalipomchukua.

Vilevile mwandishi anaonesha mgogoro wa nafsi kwa kumtumia mhusika Rosa, baada ya kukataliwa kuolewa na Charles. Mwandishi anasema;

“Ha! Rosa, kweli wewe ulikuwa bikira! Unafikiri baada ya kufahamu kwamba ulichezewa sana huko Morogoro,na baada yangu mimi mwenyewe kuona bonde la ufa na kuliona hilo sikio,unafikiri mimi ninaweza kukuoa! Ha! Dada yangu,sahau.’’uk 90

Suluhisho la mgogoro huu ni Rosa kuchukua maaamuzi ya  kujiua.

Kwa mujibu wa ki-marx migogoro haina budi kuwepo katika jamii na ni lazima pawepo migogoro ndani ya jamii yeyote, hivyo ni lazima itafutiwe suluhisho  ili kuleta maendeleo.

Vilevile suala la matabaka; matabaka ni utofauti uliopo kati ya mtu na mtu au jamii na serikali.

Katika jamii kuna matabaka ya aina mbili ambayo ni tabaka la juu na tabaka la chini katika mfumo wa uzalishaji mali yaani kiuchumi,kisiasa na kiutamaduni. Mwandishi anaonesha suala hili jinsi linavyojidhihirisha wazi kati ya wenye nacho na wasio nacho mfano familia ya Zakaria hawa ndio wasionacho uk.38, mwandishi anasema:-

‘’…Walianza kufikiri, akija atalala wapi? Mgeni-mkubwa na mwenye heshima namna hiyokulala naye ndani ya nyumba moja isiyo na vyumba vingi lilikuwa jambo la aibu.”

 Pamoja na hayo wapo wenyenavyo ni kama vile Mkuu wa wilaya Deogratus uk.41,

“Nasikia alikwisha wapa mimba watoto wawili wa shule? Ndiyo, lakini aliwapa shilingi wasimseme. Walitaja vijana wengine waliokuwa wakisoma nao.”

  Watawala mfano kiongozi Mkuu wa wilaya uk. 58 na watawaliwa ni  Zakaria na  Ndalo. Tatu,matabaka kati ya wasomi na wasiosoma, wasomi kama Rosa,Stella na Charles, wasiosoma ni Regina uk. 46.

Suala hili la matabaka katika jamii zetu bado linaendelea, hivyo kwa mtazamo wa kimarx unatoa pendekezo kuwa ili jamii ijikomboe na matabaka lazima ifanye mapinduzi.

Vilevile suala la uzalishaji mali, uzalishaji mali huo unaweza kuwa katika nyanja za kiuchumi,kisiasa,kiutamaduni na kijamii .Mfumo wa uzalishaji mali kwaujumla huzingatia katika uletaji maendeleo ya mtu binafsi au nchi kwa ujumla. Katika  riwaya  hii mwandishi anaonesha  jinsi mhusika Zakaria navyoshindwa kufuatilia vitu ambavyo vinaweza kumkomboa yeye pamoja na familia yake badala yake anaendekeza ulevi ambayo siyo njia sahihi ya uzalishaji mali. Katika uk. 17, mwandishi anasema :-

‘’Aaa! Aaa! Pombe ilikuwa ya kutuua. Hivi tulikunywa chupa ngapi? Zakaria aliuliza. Mimi nakumbuka tulikunywa chupa kumi.”

Kitendo hiki hata katika jamii zetu bado kipo kwani watu wengi hujihusisha na masuala ya ulevi kuliko kujihusisha na masuala ambayo ni tija katika uzalishaji mali.

Hivyo ili mhakiki wa kazi za kifasihi  aweze kufanya kazi yake vizuri ni lazima atumie nadharia zaidi ya moja ili aweze kuhakiki  vipengele vyote vya fani na maudhui, kwani kipengele kimoja hakiwezi kujitosheleza katika kuhakiki kazi ya kifasihi.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

MAREJELEO


 



Kezilahabi, E. (2011). Rosa Mistika. Nairobi: Kenya Literature Bureau

TUKI. (2014). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: O.U.P East Africa Limited.

Wamitila, K. (2002). Uhakiki wa Fasihi, Misingi na Vipengele vyake. Mombasa: Phoenix Publishers Limited.

 


 

 

Comments

Post a Comment